< Zaburi 71 >

1 Katika wewe, Yahwe, napatakimbilio salama; usiniache niaibishwe.
Ee Bwana, nimekukimbilia wewe, usiache nikaaibika kamwe.
2 Uniokoe na kunifanya salama katika haki yako; geuzia sikio lako kwangu.
Kwa haki yako uniponye na kuniokoa, unitegee sikio lako uniokoe.
3 Uwe kwagu mwamba kwa ajili ya kimbilio salama ambako naweza kwenda siku zote; wewe umeamuru kuniokoa, kwa kuwa wewe ni mwamba wangu na ngome yangu.
Uwe kwangu mwamba wa kimbilio, mahali nitakapokimbilia kila wakati; toa amri ya kuniokoa, kwa kuwa wewe ni mwamba wangu na ngome yangu.
4 Uniokoe mimi, Mungu wangu, kutoka katika mkono wa asiye haki na katili.
Ee Mungu wangu uniokoe kutoka kwenye mkono wa mwovu, kutoka kwenye makucha ya watu wabaya na wakatili.
5 Maana wewe ni tumaini langu, Bwana Yahwe. Nimekuamini wewe siku zote tangu nilipokuwa mtoto.
Kwa kuwa umekuwa tumaini langu, Ee Bwana Mwenyezi, tegemeo langu tangu ujana wangu.
6 Nimekuwa nikisaidiwa na wewe tangu tumboni; wewe ndiye yule uliyenitoa tumboni mwa mama yangu; sifa zangu zitakuhusu wewe siku zote.
Tangu kuzaliwa nimekutegemea wewe, ulinitoa tumboni mwa mama yangu. Nitakusifu wewe daima.
7 Mimi ni mfano bora kwa watu wangu; wewe ni kimbilio langu lenye nguvu.
Nimekuwa kama kioja kwa wengi, lakini wewe ni kimbilio langu imara.
8 Mama yangu atajawa na sifa zako, siku zote akikuheshimu.
Kinywa changu kimejazwa sifa zako, nikitangaza utukufu wako mchana kutwa.
9 Usinitupe katika siku za miaka ya uzee wangu; usiniache wakati nguvu zangu zitakapoisha.
Usinitupe wakati wa uzee, wala usiniache nguvu zangu zinapopungua.
10 Maana adui zangu wanazungumza kuhusu mimi; wale wanao fatilia uhai wangu wanapanga njama pamoja.
Kwa maana adui zangu wananisengenya, wale wanaonivizia kuniua wafanya hila.
11 Wao husema, “Mungu amemuacha; mfuateni na mumchukue, maana hakuna yeyote awezaye kumuokoa yeye.”
Wanasema, “Mungu amemwacha, mkimbilieni mkamkamate, kwani hakuna wa kumwokoa.”
12 Mungu, usiwe mbali nami; Mungu wangu, harakisha kunisaidia mimi.
Ee Mungu, usiwe mbali nami, njoo haraka kunisaidia, Ee Mungu wangu.
13 Waaibishwe na kuharibiwa, wale walio adui wa uhai wangu; wavishwe laumu na kudharauliwa, wale watafutao kuniumiza.
Washtaki wangu na waangamie kwa aibu, wale wanaotaka kunidhuru na wafunikwe kwa dharau na fedheha.
14 Lakini nitakutumainia wewe siku zote na nitakusifu wewe zaidi na zaidi.
Lakini mimi, nitatumaini siku zote, nitakusifu zaidi na zaidi.
15 Kinywa changu kitaongea kuhusu haki yako na wokovu wako mchana kutwa, ingawa ziwezi kuzielewa maana ni nyingi mno.
Kinywa changu kitasimulia haki yako, wokovu wako mchana kutwa, ingawa sifahamu kipimo chake.
16 Nitakuja na matendo yenye nguvu ya Bwana Yahwe; nitataja haki yako, yako pekee.
Ee Bwana Mwenyezi, nitakuja na kutangaza matendo yako makuu, nitatangaza haki yako, yako peke yako.
17 Mungu, tangu ujana wangu wewe umenifundisha; hata sasa ninatangaza matendo yako ya ajabu.
Ee Mungu, umenifundisha tangu ujana wangu, hadi leo ninatangaza matendo yako ya ajabu.
18 Hakika, hata niwapo mzee na mvi kichwani, Mungu, usiniache mimi, kama ambavyo nimekuwa nikitanga nguvu yako kwa vizazi vijavyo, na uweza wako kwa yeyote ajaye.
Ee Mungu, usiniache, hata niwapo mzee wa mvi, mpaka nitangaze uwezo wako kwa kizazi kijacho, nguvu zako kwa wote watakaokuja baadaye.
19 Pia haki yako, Mungu, iko juu sana; wewe ambaye umefanya mambo makuu, Mungu, ni nani aliye kama wewe?
Ee Mungu, haki yako imefika juu katika mbingu, wewe ambaye umefanya mambo makuu. Ee Mungu, ni nani aliye kama wewe?
20 Wewe ambaye umetuonesha sisi mateso mengi utatuhuisha tena na utatupandisha tena juu kutoka kwenye kina cha nchi.
Ingawa umenifanya nipate taabu, nyingi na chungu, utanihuisha tena, kutoka vilindi vya dunia utaniinua tena.
21 Uiongeze heshima yangu; rudi tena na unifariji.
Utaongeza heshima yangu na kunifariji tena.
22 Nami pia nitakushukuru kwa kinubi kwa ajili ya uaminifu wako, Mungu wangu; kwako nitaimba sifa kwa kinubi, Mtakatifu wa Israel.
Ee Mungu wangu, nitakusifu kwa kinubi kwa ajili ya uaminifu wako; Ee Uliye Mtakatifu wa Israeli, nitakuimbia sifa kwa zeze.
23 Midomo yangu itapiga kelele kwa sababu ya furaha wakati nikikuimbia sifa, hata kwa roho yangu, ambayo wewe umeikomboa.
Midomo yangu itapaza sauti kwa furaha ninapokuimbia sifa, mimi, ambaye umenikomboa.
24 Ulimi wangu pia utaongea kuhusu haki yangu mchana kutwa; maana wameaibishwa na kuvurugwa, wale waliotafuta kuniumiza.
Ulimi wangu utasimulia matendo yako ya haki mchana kutwa, kwa maana wale waliotaka kunidhuru, wameaibishwa na kufadhaishwa.

< Zaburi 71 >