< Luka 23 >
1 Mkutano wote wakasimama, wakampeleka Yesu mbele ya Pilato.
Kisha umati wote wa watu ukainuka na kumpeleka Yesu kwa Pilato.
2 Wakaanza kumshutumu, wakisema, “Tumemkuta mtu huyu akipotosha taifa letu, kwa kukataza tusitoe kodi kwa Kaisari, na akisema kwamba yeye mwenyewe ni Kristo, Mfalme.”
Nao wakaanza kumshtaki wakisema: “Tumemwona huyu mtu akipotosha taifa letu, akiwazuia watu wasilipe kodi kwa Kaisari na kujiita kuwa yeye ni Kristo, mfalme.”
3 Pilato akamuuliza, akisema, “Je wewe ni Mfalme wa Wayahudi?” Na Yesu akamjibu akisema, “Wewe wasema hivyo”.
Basi Pilato akamuuliza Yesu, “Wewe ndiye mfalme wa Wayahudi?” Yesu akajibu, “Wewe wasema.”
4 Pilato akamuambia kuhani mkuu na makutano, “Sioni kosa kwa mtu huyu”.
Pilato akawaambia viongozi wa makuhani na watu wote waliokuwepo, “Sioni sababu ya kutosha kumshtaki mtu huyu!”
5 Lakini wao wakasisitiza, wakisema, “Amekuwa akiwachochea watu, akifundisha katika Uyahudi yote, kuanzia Galilaya na sasa yuko hapa.”
Lakini wao wakakazana kusema, “Anawachochea watu kwa mafundisho yake katika Uyahudi yote, tangu Galilaya alikoanzia, hadi sehemu hii!”
6 Pilato aliposikia haya, akaulizia kama mtu huyo ni wa Galilaya?
Pilato aliposikia hayo akauliza, “Huyu mtu ni Mgalilaya?”
7 Alipotambua kuwa alikuwa chini ya utawala wa Herode, akampeleka Yesu kwa Herode, ambaye naye alikuwa Yerusalemu kwa siku hizo.
Alipofahamu kwamba Yesu alikuwa chini ya mamlaka ya Herode, akampeleka kwa Herode, ambaye wakati huo alikuwa pia Yerusalemu.
8 Herode alipomuona Yesu, alifurahi sana kwasababu alitaka kumuona kwa siku nyingi. Alisikia habari zake na alitamani kuona moja ya miujiza ikifanywa na yeye.
Herode alipomwona Yesu alifurahi sana, kwa sababu kwa muda mrefu alikuwa amesikia mambo mengi kumhusu yeye. Pia alitarajia kumwona akifanya miujiza kadha wa kadha.
9 Herode alimhoji Yesu kwa maneno mengi, lakini Yesu hakumjibu chochote.
Herode akamuuliza maswali mengi, lakini Yesu hakumjibu lolote.
10 Makuhani wakuu pamoja na waandishi walisimama kwa ukali wakimshitaki.
Wakati huo viongozi wa makuhani na walimu wa sheria walikuwepo wakitoa mashtaka yao kwa nguvu sana.
11 Herode pamoja na maaskari wake, walimtukana na kumdhihaki, na kumvika mavazi mazuri, kisha akamrudisha Yesu kwa Pilato.
Herode na askari wake wakamdhihaki Yesu na kumfanyia mzaha. Wakamvika vazi zuri sana, wakamrudisha kwa Pilato.
12 Herode na Pilato wakawa marafiki kuanzia siku hiyo, (kabla ya hapo walikuwa maadui).
Siku hiyo, Herode na Pilato wakawa marafiki; kabla ya jambo hili walikuwa na uadui kati yao.
13 Pilato akawaita pomoja makuhani wakuu na watawala na umati wa watu,
Basi Pilato akawaita pamoja viongozi wa makuhani, viongozi wengine na watu,
14 Akawaambia, “Mmeniletea mtu huyu kama mtu anaye waongoza watu wafanye mabaya, na tazama, baada ya kuwa nimemhoji mbele yenu, sikuona kosa kwa mtu huyu kuhusu mambo yote ambayo ninyi mnamshitaki yeye.
akawaambia, “Ninyi mlimleta huyu mtu kwangu kana kwamba ni mtu anayewachochea watu ili waasi. Nimemhoji mbele yenu nami nimeona hakuna msingi wowote wa mashtaka yenu dhidi yake.
15 Hapana, wala Herode, kwa maana amemrudisha kwetu, na tazama hakuna chochote alichokifanya kinachostahili adhabu ya kifo.
Wala Herode hakumwona na kosa lolote, ndiyo sababu amemrudisha kwetu. Kama mnavyoona, mtu huyu hakufanya jambo lolote linalostahili kifo.
16 Kwahiyo basi nitamuadhibu na kumuachilia.
Kwa hiyo nitaamuru apigwe mijeledi na kumwachia.” [
17 (Sasa, Pilato anawajibika kumuachilia mfungwa mmoja kwa wayahudi wakati wa sikukuu).
Kwa kuwa ilikuwa lazima kuwafungulia mfungwa mmoja wakati wa Sikukuu.]
18 Lakini wote wakapiga kelele pamoja, wakisema, “Mwondoe huyo, na tufungulie Baraba!”
Ndipo watu wote wakapiga kelele kwa pamoja, “Mwondoe mtu huyo! Tufungulie Baraba!”
19 Baraba alikuwa ni mtu ambaye amewekwa gerezani kwa sababu ya uasi fulani katika jiji na kwa kuua.
(Baraba alikuwa amefungwa gerezani kwa sababu ya maasi yaliyokuwa yametokea mjini, na kwa ajili ya uuaji.)
20 Pilato akawaambia tena, akitamani kumwachilia Yesu.
Pilato, akitaka kumwachia Yesu, akasema nao tena.
21 Lakini wao wakapiga kelele, wakisema, “Msulibishe, msulibishe.”
Lakini wao wakaendelea kupiga kelele wakisema, “Msulubishe! Msulubishe!”
22 Akawauliza kwa mara ya tatu, “kwa nini, huyu mtu amefanya maovu gani? Sikupata kosa linalostahili adhabu ya kifo kwake. Kwahiyo nitakapo maliza kumuadhibu nitamuachilia.”
Kwa mara ya tatu, Pilato akawauliza, “Kwani amefanya kosa gani huyu mtu? Sikuona kwake sababu yoyote inayostahili adhabu ya kifo. Kwa hiyo nitaamuru apigwe mijeledi, na kisha nitamwachia.”
23 Lakini wakasisitiza kwa sauti ya juu, wakitaka asulubiwe. Na sauti zao zikamshawishi Pilato.
Lakini watu wakazidi kupiga kelele kwa nguvu zaidi, wakidai kwamba Yesu asulubiwe. Hivyo, kelele zao zikashinda.
24 Hivyo Pilato akaamua kuwapatia matakwa yao.
Kwa hiyo Pilato akatoa hukumu kwamba madai yao yatimizwe.
25 Akamuachilia yule waliyemtaka ambaye alifungwa kwa kusababisha ghasia na kuua. Lakini akamtoa Yesu kwa matakwa yao.
Akamfungua yule mtu aliyekuwa amefungwa gerezani kwa kuhusika katika uasi dhidi ya serikali na mauaji. Akamkabidhi Yesu mikononi mwao, wamfanyie watakavyo.
26 Walipokuwa wakimpeleka, walimkamata mtu mmoja aitwaye Simoni wa Ukirene, akitokea katika nchi, wakamtwika msalaba ili abebe, akimfuata Yesu.
Walipokuwa wakienda naye, wakamkamata mtu mmoja aitwaye Simoni mwenyeji wa Kirene, aliyekuwa anapita zake kuingia mjini kutoka shambani. Wakambebesha msalaba, wakamlazimisha auchukue nyuma ya Yesu.
27 umati mkubwa wa watu, na wanawake ambao walihuzunika na kuomboleza kwa ajili yake, walikuwa wakimfuata.
Idadi kubwa ya watu wakamfuata Yesu, wakiwamo wanawake waliokuwa wakimlilia na kumwombolezea.
28 Lakini akawageukia, Yesu akawaambia, 'Mabinti wa Yerusalemu, msinililie mimi, bali jililieni ninyi wenyewe na kwa ya ajili watoto wenu.
Yesu akawageukia, akawaambia, “Enyi binti za Yerusalemu, msinililie mimi bali jililieni ninyi wenyewe na watoto wenu.
29 Tazama, siku zinakuja ambazo watasema, “Wamebarikiwa walio tasa na matumbo yasiyozaa, na matiti ambayo hayakunyonyesha.
Kwa maana wakati utafika mtakaposema, ‘Wamebarikiwa wanawake tasa, ambao matumbo yao hayakuzaa, wala matiti yao hayakunyonyesha!’
30 Ndipo watakapo anza kuiambia milima, 'Tuangukieni,' na vilima, 'Mtufunike.'
Ndipo “‘wataiambia milima, “Tuangukieni!” na vilima, “Tufunikeni!”’
31 Maana kama wakifanya mambo haya ikiwa mti mbichi, itakuwaje ukiwa mkavu?”
Kwa maana kama wamefanya hivi kwa mti mbichi, kwa mti mkavu itakuwaje?”
32 wanaume wengine, wahalifu wawili, walipelekwa pamoja naye ili wauwawe.
Watu wengine wawili wahalifu, walipelekwa pamoja na Yesu ili wakasulubiwe.
33 Walipofika mahali paitwapo Fuvu la kichwa, ndipo wakamsulubisha pamoja na wale wahalifu, mmoja upande wa kulia na mwingine upande wa kushoto.
Walipofika mahali paitwapo Fuvu la Kichwa, hapo ndipo walipomsulubisha Yesu pamoja na hao wahalifu, mmoja upande wake wa kuume na mwingine upande wake wa kushoto.
34 Yesu alisema, “Baba, uwasamehe, kwa kuwa hawajui watendalo. “Nao wakapiga kura, kugawa mavazi yake.
Yesu akasema, “Baba, wasamehe, kwa maana hawajui walitendalo!” Wakagawana nguo zake kwa kupiga kura.
35 Watu walikuwa wamesimama wakiangalia huku watawala wakimdhihaki, wakisema, “Aliwaokoa wengine. Sasa ajiokoe mwenyewe, kama yeye ni Kristo wa Mungu, mteule”.
Watu wakasimama hapo wakimwangalia, nao viongozi wa Wayahudi wakamdhihaki wakisema, “Aliokoa wengine! Ajiokoe mwenyewe basi, kama yeye ndiye Kristo wa Mungu, Mteule wake.”
36 Askari pia walimdharau, walimkaribia yeye na wakumpa siki,
Askari nao wakaja, wakamdhihaki. Wakamletea siki ili anywe,
37 wakisema, “Kama wewe ni Mfalme wa Wayahudi jiokoe mwenyewe”
na wakamwambia, “Kama wewe ni Mfalme wa Wayahudi, jiokoe mwenyewe.”
38 Kulikuwa pia na alama juu yake iliyoandikwa “HUYU NDIYE MFALME WA WAYAHUDI.”
Kwenye msalaba juu ya kichwa chake, kulikuwa na maandishi haya: Huyu ndiye Mfalme wa Wayahudi. Maandishi haya yalikuwa yameandikwa kwa lugha za Kiyunani, Kilatini na Kiebrania.
39 Mmoja wa wahalifu aliyesulubishwa alimtukana akisema, “Wewe si Kristo? jiokoe mwenyewe na sisi”
Mmoja wa wale wahalifu waliosulubiwa pamoja naye akamtukana, akasema: “Wewe si ndiye Kristo? Jiokoe mwenyewe na utuokoe na sisi.”
40 Lakini yule mwingine akajibu, akimkemea na akisema, “Je wewe humuogopi Mungu, nawe uko katika hukumu hiyo hiyo?
Lakini yule mhalifu mwingine akamkemea mwenzake, akasema, “Je, wewe humwogopi Mungu, wakati uko kwenye adhabu iyo hiyo?
41 Sisi tupo hapa kwa haki, kwa maana sisi tunapokea kile tunachostahili kwa matendo yetu. Lakini mtu huyu hakufanya chochote kibaya.”
Sisi tumehukumiwa kwa haki kwa kuwa tunapata tunayostahili kwa ajili ya matendo yetu. Lakini huyu mtu hajafanya kosa lolote.”
42 Na aliongeza, “Yesu, nikumbuke utakapoingia katika ufalme wako.”
Kisha akasema, “Yesu, unikumbuke utakapokuja katika Ufalme wako.”
43 Yesu akamwambia, “Amini nakuambia, leo hii utakuwa pamoja nami Paradiso.”
Yesu akamjibu, “Amin, nakuambia, leo hii utakuwa pamoja nami Paradiso.”
44 Hapo ilikuwa karibu saa ya sita, giza likaja juu ya nchi yote hadi saa ya tisa,
Ilikuwa kama saa sita mchana, nalo giza likafunika nchi yote hadi saa tisa,
45 Mwanga wa jua ulizimika. Kisha pazia la hekalu likagawanyika katikati kuanzia juu.
kwa sababu jua liliacha kutoa nuru. Pazia la Hekalu likachanika vipande viwili.
46 Akilia kwa sauti kuu, Yesu alisema, “Baba mikononi mwako naiweka roho yangu,” baada ya kusema haya, akafa.
Yesu akapaza sauti yake akasema, “Baba, mikononi mwako naikabidhi roho yangu.” Baada ya kusema haya, akakata roho.
47 Wakati Akida alipoona yaliyotendeka alimtukuza Mungu akisema, “Hakika huyu alikuwa mtu mwenye haki.”
Yule jemadari alipoona yaliyotukia, akamsifu Mungu, akasema, “Hakika, mtu huyu alikuwa mwenye haki.”
48 Wakati umati wa watu waliokuja pamoja kushuhudia walipoona mambo yaliyofanyika, walirudi huku wakipiga vifua vyao.
Watu wote waliokuwa wamekusanyika hapo kushuhudia tukio hili walipoyaona hayo, wakapigapiga vifua vyao kwa huzuni na kwenda zao.
49 Lakini marafiki zake, na wanawake waliomfuata toka Galilaya, walisimama kwa mbali wakiangalia hayo mambo.
Lakini wale wote waliomfahamu, pamoja na wale wanawake waliokuwa wamemfuata kutoka Galilaya, walisimama kwa mbali wakiyatazama mambo haya.
50 Tazama, palikuwepo na mtu aitwaye Yusufu, ambaye ni mmoja wa baraza, mtu mzuri na mwenye haki,
Basi kulikuwa na mtu mmoja mwema na mwenye haki, jina lake Yosefu. Yeye alikuwa mjumbe wa Baraza la Wayahudi,
51 (alikuwa hajakubaliana na maamuzi au matendo yao), kutoka Armathaya, mji wa Kiyahudi, ambao ulikua ukisubiria ufalme wa Mungu.
lakini yeye hakuwa amekubaliana na maamuzi na vitendo vya viongozi wenzake. Huyu alikuwa mwenyeji wa Arimathaya huko Uyahudi, naye alikuwa anaungojea Ufalme wa Mungu kwa matarajio makubwa.
52 Mtu huyu, alimkaribia Pilato, akaomba apewe mwili wa Yesu.
Yosefu alikwenda kwa Pilato, akaomba apewe mwili wa Yesu.
53 Alimshusha, na akauzungushia sanda, na akaumweka katika kaburi lililokuwa limechongwa katika jiwe, ambalo hakuna aliyewahi kuzikwa.
Akaushusha kutoka msalabani, akaufunga katika kitambaa cha kitani safi, na kuuweka katika kaburi lililochongwa kwenye mwamba, ambalo halikuwa limezikiwa mtu mwingine bado.
54 Ilikuwa ni siku ya maandalizi, na Sabato inakaribia.
Ilikuwa Siku ya Maandalizi, nayo Sabato ilikuwa karibu kuanza.
55 Wanawake, waliokuja nao kutoka Galilaya, walimfuata, na wakaona kaburi na jinsi mwili wake ulivyolazwa.
Wale wanawake waliokuwa wamekuja pamoja na Yesu wakimfuata kutoka Galilaya wakamfuata Yosefu, wakaliona kaburi na jinsi mwili wa Yesu ulivyolazwa.
56 Walirudi na kuanza kuandaa manukato na marashi. Kisha siku ya sabato walipumzika kwa mujibu wa sheria.
Kisha wakarudi nyumbani, wakaandaa manukato na marhamu ya kuupaka huo mwili. Lakini wakapumzika siku ya Sabato kama ilivyoamriwa.