< Zaburi 62 >
1 Kwa mwimbishaji. Mtindo wa Yeduthuni. Zaburi ya Daudi. Kwa Mungu peke yake nafsi yangu inapata pumziko; wokovu wangu watoka kwake.
Katika ukimya ninamsubiri Mungu pekee; wokovu wangu watoka kwake.
2 Yeye peke yake ndiye mwamba wangu na wokovu wangu; yeye ni ngome yangu, sitatikisika kamwe.
Yeye pekee ni mwamba wangu na wokovu wangu; yeye ni mnara wangu mrefu; sitasogezwa kamwe.
3 Mtamshambulia mtu hata lini? Je, ninyi nyote mtamtupa chini, ukuta huu ulioinama na uzio huu unaotikisika?
Mpaka lini, ninyi nyote, mtamshambulia mtu, ili kwamba mumpindue yeye kama ukuta ulio inama au kama fensi isiyo imara?
4 Walikusudia kikamilifu kumwangusha toka mahali pake pa fahari; wanafurahia uongo. Kwa vinywa vyao hubariki, lakini ndani ya mioyo yao hulaani.
Wanashauliana naye ili tu kumshusha chini kutoka kwenye nafasi yake heshimiwa; wao wanapenda kuongea uongo; wanambariki yeye kwa midomo yao, lakini mioyoni mwao wana mlaani yeye. (Selah)
5 Ee nafsi yangu, upumzike, kwa Mungu peke yake, tumaini langu latoka kwake.
Katika ukimya ninamsubiri Mungu pekee; kwa maana matumaini yangu yako kwake.
6 Yeye peke yake ndiye mwamba wangu na wokovu wangu; ndiye ngome yangu, sitatikisika.
Yeye pekee ni mwamba wangu na wokovu wangu; yeye ni mnara wangu mrefu; sitasogezwa.
7 Wokovu wangu na heshima yangu viko kwa Mungu, ndiye mwamba wangu wenye nguvu na kimbilio langu.
Na Mungu ni wokovu wangu na utukufu wangu; mwamba wa nguvu yangu na kimbilio langu salama liko katika Mungu.
8 Enyi watu, mtumainini yeye wakati wote, miminieni mioyo yenu kwake, kwa kuwa Mungu ni kimbilio letu.
Mwaminini Mungu wakati wote, ninyi watu; mimina moyo wako mbele zake; Mungu ni kimbilio salama kwa ajili yetu. (Selah)
9 Binadamu wa ngazi ya chini ni pumzi tu, nao wa ngazi ya juu ni uongo tu; wakipimwa kwenye mizani, si chochote; wote kwa pamoja ni pumzi tu.
Hakika watu wenye msimamo mdogo ni ubatili, na watu wenye msimamo mkubwa ni waongo; wao watakuwa wepesi kwenye mzani; uzito wao pamoja ni wepesi kuliko kitu chochote.
10 Usitumainie vya udhalimu wala usijivune kwa vitu vya wizi; ingawa utajiri wako utaongezeka, usiviwekee moyo wako.
Usiamini katika ukandamizaji au wizi; usitumainie utajiri, maana hawatazaa matunda; usiuweke moyo wako kwenye hivyo.
11 Jambo moja Mungu amelisema, mambo mawili nimeyasikia: kwamba, Ee Mungu, wewe una nguvu,
Mungu ameongea mara moja, mara mbili nimesikia hili: nguvu ni za Mungu.
12 na kwamba, Ee Bwana, wewe ni mwenye upendo. Hakika utampa kila mtu thawabu kwa kadiri ya alivyotenda.
Pia kwako, Bwana, ni uaminifu wa agano, maana humlipa kila mtu kwa kile alichokifanya.