< Zaburi 62 >

1 Kwa mwimbishaji. Mtindo wa Yeduthuni. Zaburi ya Daudi. Kwa Mungu peke yake nafsi yangu inapata pumziko; wokovu wangu watoka kwake. 2 Yeye peke yake ndiye mwamba wangu na wokovu wangu; yeye ni ngome yangu, sitatikisika kamwe. 3 Mtamshambulia mtu hata lini? Je, ninyi nyote mtamtupa chini, ukuta huu ulioinama na uzio huu unaotikisika? 4 Walikusudia kikamilifu kumwangusha toka mahali pake pa fahari; wanafurahia uongo. Kwa vinywa vyao hubariki, lakini ndani ya mioyo yao hulaani. 5 Ee nafsi yangu, upumzike, kwa Mungu peke yake, tumaini langu latoka kwake. 6 Yeye peke yake ndiye mwamba wangu na wokovu wangu; ndiye ngome yangu, sitatikisika. 7 Wokovu wangu na heshima yangu viko kwa Mungu, ndiye mwamba wangu wenye nguvu na kimbilio langu. 8 Enyi watu, mtumainini yeye wakati wote, miminieni mioyo yenu kwake, kwa kuwa Mungu ni kimbilio letu. 9 Binadamu wa ngazi ya chini ni pumzi tu, nao wa ngazi ya juu ni uongo tu; wakipimwa kwenye mizani, si chochote; wote kwa pamoja ni pumzi tu. 10 Usitumainie vya udhalimu wala usijivune kwa vitu vya wizi; ingawa utajiri wako utaongezeka, usiviwekee moyo wako. 11 Jambo moja Mungu amelisema, mambo mawili nimeyasikia: kwamba, Ee Mungu, wewe una nguvu, 12 na kwamba, Ee Bwana, wewe ni mwenye upendo. Hakika utampa kila mtu thawabu kwa kadiri ya alivyotenda.

< Zaburi 62 >