< Isaya 46 >

1 Beli anasujudu hadi nchi, Nebo anainama; sanamu zao zabebwa na wanyama wa mizigo. Vinyago hivi mnavyobeba kila mahali ni mzigo wa kulemea, mzigo kwa waliochoka. 2 Vinyago pamoja na wale wanaovibeba wanainama chini; hiyo miungu haiwezi kuwaokoa watu, wote wanakwenda utumwani pamoja. 3 “Nisikilizeni mimi, ee nyumba ya Yakobo, ninyi nyote mliobaki wa nyumba ya Israeli, ninyi ambao nimewategemeza tangu mlipotungwa mimba, nami nimewabeba tangu kuzaliwa kwenu. 4 Hata mpaka wakati wa uzee wenu na mvi, Mimi ndiye, Mimi ndiye nitakayewasaidia ninyi. Nimewahuluku, nami nitawabeba, nitawasaidia ninyi na kuwaokoa. 5 “Mtanilinganisha na nani, au mtanihesabu kuwa sawa na nani? Ni nani mtakayenifananisha naye ili tuweze kulinganishwa? 6 Wengine humwaga dhahabu kutoka kwenye mifuko yao, na kupima fedha kwenye mizani; huajiri mfua dhahabu kutengeneza mungu, kisha huisujudia na kuiabudu. 7 Huiinua mabegani na kuichukua; huiweka mahali pake, papo hapo ndipo isimamapo. Wala haiwezi kusogea kutoka mahali pale. Ingawa mtu huililia, haimjibu; haiwezi kumwokoa kwenye taabu zake. 8 “Kumbukeni hili, litieni akilini, liwekeni moyoni, enyi waasi. 9 Kumbukeni mambo yaliyopita, yale ya zamani za kale; mimi ndimi Mungu, wala hakuna mwingine; mimi ndimi Mungu, wala hakuna mwingine aliye kama mimi. 10 Ni mimi nitangazaye mwisho tangu mwanzo, naam, tangu zamani za kale, mambo ambayo hayajatendeka. Ninasema: Kusudi langu ndilo litakalosimama, nami nitatenda mapenzi yangu yote. 11 Kutoka mashariki ninaita ndege awindaye; kutoka nchi ya mbali, mtu atakayetimiza kusudi langu. Lile ambalo nimelisema, ndilo nitakalolitimiza; lile nililolipanga, ndilo nitakalolitenda. 12 Nisikilizeni, ninyi wenye mioyo migumu, ninyi mlio mbali na haki. 13 Ninaleta haki yangu karibu, haiko mbali; wala wokovu wangu hautachelewa. Nitawapa Sayuni wokovu, Israeli utukufu wangu.

< Isaya 46 >